Friday, 5 May 2017

Faida za wanaume kuongozana na wake zao kliniki.



https://blogger.googleusercontent.com/img/b/R29vZ2xl/AVvXsEjnt7ADqvbbb3olBOnaqx4qoiSAh4bk0SSWHfIwxB4afYMXT7_FJ8heKDopG5NRdM5O6UIf3e6b4TJ8hZ8S8YTy2SdUuYRBRbmbphnbrYbI5JUFVS4wiLYdQi7BvP7mgl8_Q_YZsL7tp-Q/s1600/kliniki.jpg
Kuna dhana  imejengeka nchini  miongoni mwa wanaume kwamba ni wanawake pekee ndio wenye wajibu wa kuhudhuria kliniki wakati wa ujauzito na  baada ya kujifungua.

Katika miaka ya karibuni kuna  kampeni kubwa ya kuwataka wanaume waongozane na wenza wao  kliniki ili kwa ajili ya kupata ushauri wa kitaalam kuhusu afya ya uzazi. Makala hii yafafanua zaidi

“KUTOKANA na mila na desturi, binafsi nilipanga kuzaa  watoto watano. Hata hivyo, mume wangu anaonekana kuwa kinyume na mawazo yangu na amekuwa mara zote akisisitiza kwamba angependa tuzae watoto watatu tu,” anasema moja ya Mama aliekuja kliniki nilipomhoji..

Wakati wa mahojiano haya alikuwa kwenye foleni ya kusubiri huduma ya kliniki katika hospitali moja hivi. anasema kwamba hadi sasa yeye na mume wake ambaye ni Mkulima wamefanikiwa kupata watoto wawili ambao wametofautiana  kwa  miaka miwili.

Anasema kwamba, tangu alipoolewa amekuwa na mawazo ya kuzaa watoto watano akiamini kwamba atakuwa amezingatia uzazi wa mpango. Katika familia yake wamezaliwa  watoto 12.

Hata hivyo anasema kwamba ,anaona kila dalili kuwa ndoto yake ya kuzaa  watoto watano huenda isitimie kutokana na msimamo wa  mume wake.

Anabainisha kuwa, chanzo cha mume wake kuwa na msimamo wa kuzaa watoto wasiozidi watatu ni baada ya kuhudhuria kliniki na kushauriwa  kufanya hivyo.

“Unajua siku hizi akina mama tunapohudhuria kliniki tunashauriwa kufuatana na wenza wetu. Nilipomuambia mume wangu alikubali bila kusita,”anasema.

Anaongeza kuwa, tangu siku ya kwanza alipohudhuria kliniki, mume wake ameonekana kufanyia kazi ushauri waliopewa na wataalam wa  afya ya uzazi ikiwemo  kuzaa idadi ndogo ya watoto  watakaoweza kuwatunza.

Anasema kwamba licha ya kutumia muda mwingi akiwa katika shughuli zake za ukulima, lakini anapokuwa nyumbani mume wake hufuatana naye kwenda kliniki kwa ajili ya kupima ujauzito au mtoto na  hufundishwa jinsi ya kuzuia maambukizo ya Virusi vya Ukimwi kutoka  mama kwenda kwa mtoto.

Kwa mujibu wa Mama huyo, hatua hiyo ya mumewe kukubali kuambatana naye kwenda kliniki imeimarisha ndoa yao kwa sababu kila kitu kuhusu uzazi wanakifanya kwa kushirikiana na kwa kuzingatia ushauri wa kitaalam.

“Unajua wanaume wengi wana hulka ya kutopenda kujihusisha kwa karibu na masuala ya afya ya uzazi.Wanapenda  kutuacha sisi wanawake  twende kliniki peke yetu. Inakuwa vigumu kufanyia kazi ushauri wote tunaopewa kwa sababu wengi wetu hatuna kauli kwa waume zetu,”anasema.

Anafafanua kwamba, kwa mila na desturi za kabila la wasukuma mwanamke hana mamlaka ya kumpa maelekezo mumewe, hivyo imekuwa vigumu wanawake kufikisha  ushauri waliopewa kliniki kwa wenza wao.

Hata hivyo anasema kwamba, kwake  hali ni tofauti kwa sababu uamuzi  wa  mumewe kukubali kuongozana naye kwenda kliniki kimemsaidia kupata ushauri moja kwa moja kutoka kwa wataalam na amekuwa akiufanyia kazi.

“Mimi na mume wangu tunaishi kwa maelewano hasa linapokuja suala la afya ya uzazi. Hakuna mahali tunabishana kwa sababu kila mtu anajua wajibu wake kwa kuzingatia ushauri tunaopewa kliniki. Sasa sina simanzi tena kuhusu mapenzi kwa sababu namuamini mume wangu na yeye ananiamini,”anasisitiza.

Pascal Emmanuel (19) mkazi wa kijiji cha kisuke wilayani kahama, ambaye amemaliza kidato cha nne mwaka jana (2012) alionekana  ameongozana na msichana mdogo wa rika lake  kwenda  katika kliniki ya hospitali ya wilaya hiyo.

Pascal alisema  amefika kliniki kwa ajili ya kumsindikiza mwenza wake mwenye  ujauzito wa miezi sita.

Anasema kwamba, kimsingi wao si mume na mke kama ambavyo ingeweza kudhaniwa isipokuwa wamekuwa na uhusiano wa kimapenzi tu huku kila mtu anaishi nyumbani kwa wazazi wake.
pascal anasema  amemaliza kidato cha nne mwaka jana, mwenza wake aitwaye Tatu Mabiti ameishia darasa la saba, na walipoanza  uhusiano wa kimapenzi wakajikuta wametengeneza ujauzito usiotarajiwa.

Hata hivyo, hali hiyo haijawa kikwazo kwa pascal kushirikiana na rafiki yake huyo  kulea mimba kwa kuzingatia ushauri wa kitaalam kuhusu afya ya uzazi ikiwemo kinga ya maambukizi ya VVU kutoka mama kwenda kwa mtoto.

Anasema kuwa, mara tu alipoambiwa na mwenza wake kwamba wanatakiwa kwenda pamoja kliniki, hakuhisi ubaya wowote badala yake alikubali, na siku ilipowadia wakaongozana kwenda kupata ushauri wa kitaalam kuhusu afya ya uzazi.

Anabainisha kwamba , licha ya kuambiwa na mwenza wake, kilichomsukuma kwenda kliniki ni taarifa kuhusu afya ya uzazi ambazo amekuwa akizipata kupitia matangazo mbalimbali ya redio, televisheni na machapisho.

“Nimekuwa nikisikia na hata kuona matangazo yanayosema kwamba mwanamke anapopata ujauzito tangu siku ya kwanza anapaswa kuongozana na mwenza wake kwenda kliniki, kwa hiyo hata mimi Tatu aliponiambia tuje niliona ni sawa tu,”anasema.

Anaongeza kwamba, kuongozana na mwenza wake kliniki kumemsaidia kufahamu mambo mengi kuhusu afya ya uzazi, kwa sababu kuna  baadhi ya mambo  hayapo kwenye matangazo lakini ukifika kliniki unayapata.

Aidha anasema kwamba, kitu kingine alichojifunza ni kwamba mjamzito anapoongozana na mwenza wake kliniki anahudumiwa kwa haraka zaidi tofauti na wale  wanaokwenda bila wenza wao.

“Kuna kitu hapa kimenifurahisha kwani ingawa nimekuja na mwenzangu tukiwa tumechelewa kidogo lakini tulipofika tu mara moja tumepokelewa na kupewa huduma. Hali hii imenipa somo kwamba wanawake wanaosindikizwa kliniki na wenza wao hawapati adha ya kukaa kwenye foleni,”anasema.

Mwalimu Mkuu wa shule ya msingi Kapela wilayani Bukombe Bi Tekla Manyanda anaunga mkono hoja hiyo  kwamba, hata yeye wakati akiwa mjamzito hadi alipojifungua alijitahidi kumbumbusha Mme kumsindikiza kliniki  ili  kumuwezesha kupata huduma kwa haraka nae alifanya hivyo.

Anasema kwamba, licha ya kupata huduma kwa haraka lakini kuhudhuria kliniki na mme wake kumewasaidia kujua mbinu nyingi za kupanga uzazi ambazo hazina athari kwao wala kwa watoto.

“Nilipokuwa namsindikiza mke wangu kliniki nilijifunza mambo mengi sana, kwanza tulipokuwa tunafika tulihudumiwa kwa haraka bila kujali kama tumewakuta wengine wasio na wenza wao.Pia  imetusaidia kupanga vizuri uzazi tofauti na huko nyuma nilipokuwa siendi kliniki” alisema Mme wa Mwalimu Mkuu.

Kuna mambo mengine tulikuwa hatuyazingatii kwa sababu haikuwa rahisi kwa mke wangu kukumbuka na kuniambia kila kitu alichoelezwa na wataalam,”anasema Mme wa Mwalimu Mkuu.

Neema Dismas (25) mkazi wa Dodoma anasema kwamba, ingawa inatokea mara chache, lakini anapoongozana na mumewe  kliniki hujisikia fahari sana  mbele ya wanawake wenzake.

“Natamani muda wote anapokuwa nyumbani tuongozane kwenda kliniki kwa sababu najisikia fahari.Lakini  pia kuna ushauri kuhusu afya ya uzazi  tunaopewa pamoja inakuwa rahisi kuutekeleza,”anasema.

Muuguzi Kiongozi katika kliniki iliyopo hospitali ya wilaya ya Bukombe Bi Sofia Herman anasema kwamba siku zote wamekuwa wakiwasisitiza wanawake wajawazito na wenye watoto kuambatana na wenza wao pindi wanapofika kliniki.

Anasema sababu kubwa ni kuwezesha wenza wote wawili kupata ushauri wa kitaalam kuhusu afya ya uzazi ikiwemo uzazi wa mpango na kinga ya maambukizo kutoka kwa mama kwenda kwa mtoto.

Anasema kwamba, wakati wa kliniki akina mama hufanyiwa vipimo mbalimbali vikiwemo vya magonjwa ya zinaa na wale wanaobainika kuambukizwa hupatiwa matibabu bure.

Kwa msingi huo, anasema kwamba mama anapokuwa ameongozana na mwenza wake inakuwa rahisi kupewa ushauri wa kitaalam ili kuzuia maambukizo zaidi.

“Kuna baadhi ya kina mama tunapowapima tunabaini wameambukizwa magonjwa ya zinaa.  Kwa sababu  wanakuja peke yao inakuwa vigumu kupata tiba sahihi  hata kama tukimtibu yeye bado akirudi kwa mumewe anaweza kuambukizwa tena,”anasema.

Anatoa mfano kwamba, hivi karibuni mama mmoja alipimwa na kukutwa ameambukizwa ugonjwa wa kaswende, wakamshauri akamlete  mumewe ili naye apimwe kisha wapatiwe tiba kwa pamoja.

Hata hivyo anasema kwamba, mama huyo alipokwenda kumwambia mumewe kuwa anahitajika kliniki aligoma kwenda huku akidai kuwa  hajisikii kuumwa chochote.

Anabainisha kuwa, ndiyo sababu mara zote wamekuwa wakiwasisitiza akina mama kuongozana na wenza wao ili kama kuna jambo lolote linalohitaji ufumbuzi wa pamoja iwe rahisi kulifanyia kazi.

“Mara nyingi wanaume wanaposhindwa kuja kliniki huwa hawazingatii ushauri tunaowapa wake zao hali ambayo huchangia sio tu kuzaa watoto bila mpangilio lakini pia maambukizo zaidi ya magonjwa ya zinaa na hata virusi vya Ukimwi,”anasisitiza.

Anaongeza kwamba, wanawake ambao hawaongozani na wenza wao kliniki imekuwa vigumu kupata huduma nzuri katika kipindi cha ujauzito au malezi ya mtoto kwa sababu anayemiliki uchumi (mume) anakuwa hajui chochote kuhusu afya ya uzazi.

“Hapa wilayani Bukombe wanaume wengi ndio wanaomiliki uchumi, hivyo wanaposhindwa kuja kliniki inakuwa vigumu kuwahudumia kikamilifu wake zao katika kipindi cha ujauzito kwa sababu hawana elimu kuhusu afya ya uzazi, matokeo yake baadhi yao hupoteza maisha wakati wa kujifungua,”anasema.

Anaongeza kwamba ili kuhakikisha wanawake wanakwenda kliniki na waume zao, wameweka utaratibu kwamba anayekwenda na mwenza wake anapewa kipaumbele katika huduma, hata kama amewakuta wenzake  atahudumiwa kwanza.

Anashauri kwamba, wanaume wajitahidi kuongozana na wenza wao kliniki kwa sababu inasaidia kupatikana kwa huduma ya uhakika na haraka hospitalini na nyumbani, na kwamba kliniki ni kwa ajili ya baba, mama na mtoto.

Mratibu wa Huduma ya Afya ya Uzazi na Mtoto wilayani bukombe anasema kwamba, wanaume wengi katika wilaya hiyo hawana mwamko wa kuwasindikiza wake zao kliniki.

Wachache ambao wamepata mwamko wa kuwasindikiza wake zao kliniki anasema, wamekuwa na mafanikio makubwa katika suala zima la afya ya uzazi hata kumudu kuzaa watoto wachache wanaoweza kuwatunza na  kuzuia mapema maambukizo ya VVU kutoka mama kwenda kwa mtoto.

Anasema kwamba wanaume wasiohudhurii kliniki na wake zao wamejikuta wakizaa watoto wengi wanaoshindwa kuwatunza kwa kuwapa chakula bora na kuwapeleka shule.

“Hapa Bukombe kuna mtazamo kwamba kuzaa watoto wengi ni fahari, hivyo utakuta wanawake wengi wenye umri kati ya miaka 25 hadi 40 tayari  wamebeba mimba kati ya mara 6 hadi 8, na wengine mara 10 hadi 13,”anasema.

Hata hivyo, anasema kwamba wengi wao wamejikuta mimba zikitoka kutokana na kushindwa kuzingatia ushauri wa kitaalam kuhusu afya ya uzazi.
Hivyo Basi ni vizuri kushirikiana Baba na mama
Kuhudhuria kliniki ili kupata ushauri wa kia afya kuhusiana na uzazi wa mpango na mambo mengine yanayoshiana na ushauri wa kina
Kuhusu afya ya mama na mtoto wakati wa ujauzito.

No comments

Post a Comment